Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Mhe. Thobias Andengenye amezindua mradi wa kujenga Ustahimilivu wa Mabadiliko ya Hali ya Tabia Nchi mkoani hapa, akimwakilisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mha. Yusuf Masauni.
Uzinduzi huo umefanyika leo Mei 15, 2025 katika Hoteli ya Lake Tanganyika iliyopo Manispaa ya Kigoma Ujiji, ambapo mradi huo unalenga kukabiliana na changamoto za athari za kimazingira mkoani hapa kupitia urejeshwaji wa misitu kwa kupanda miti katika maeneo yaliyoathiriwa na ukataji holela wa miti na uharibifu wa mazingira.
Akizungumza kwenye uzinduzi huo, Andengenye amesema mkoa unahifadhi zaidi ya wakimbizi 1900,000 kutoka nchi jirani za Burundi na Congo DR, kutokana na kutoimarika kwa hali ya utulivu na amani ambapo katika maeneo wanayoishi kumeshuhudiwa uharibifu mkubwa wa mazingira ikiwemo ukataji miti kwa ajili ya nishati, kuandaa maeneo ya kilimo na shughuli nyinginezo za kibinadamu.Ameutaja mradi huo kuwa na manufaa makubwa katika matumizi bora ya Ardhi, uhimilivu wa mazingira kwa viumbe hai, kurejesha mfumo wa kiikolojia, usawa wa kijinsia katika muktadha wa kimazingira pamoja na kuendeleza sera ya Taifa katika uhifadhi wa mazingira.
Kupitia hotuba yake, kwaniaba ya waziri Masauni, Andengenye ameushukuru uongozi wa Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa(UNEP) pamoja na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) kwa kuendelea kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuwezesha na kufanikisha mradi huo unaoratibu shughuli za uhifadhi wa Mazingira kwa manufaa ya mkoa wa Kigoma na nchi kwa ujumla.
Kamilembe Mutasa Mkurugenzi wa Mazingira Ofisi ya Makamu wa Rais wa Rais (Muungano na Mazingira) amesema mradi huo wenye Thamani ya Shilingi Bil. 54 unatarajiwa kutekelezwa kwa kipindi cha Miaka mitano(5) katika wilaya za Kasulu, Kibondo na Kakonko.
Amesema Kigoma ni mkoa unaokabiliwa na athari kubwa za uharibifu wa Mazingira ambazo zinazochangiwa na shughuli za kibinadamu haswa katika maeneo yanayohifadhi wakimbizi.Amezitaja athari zinazotokana na mabadiliko ya tabia nchi kuwa ni pamoja na ongezeko la mvua, hali joto, mafuriko pamoja na ukame.
MKOA WA KIGOMA
Anuani: S.L.P 125
Simu: 0282802330
Simu ya kiganjani: +255766853404
Barua Pepe: ras@kigoma.go.tz / ras.kigoma@tamisemi.go.tz / info@kigoma.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Kigoma. Haki zote zimehifadhiwa